Searching...
Image and video hosting by TinyPic
18 October 2014
Saturday, October 18, 2014

Uchambuzi: QPR VS LIVERPOOL LEO SAA 9:30



Na Chikoti Cico

Queens Park Rangers iliyoko katika jiji la London itaikaribisha Liverpool kwenye uwanja wake wa nyumbani, Loftus Road majira ya saa 9:30 kujaribu kutafuta ushindi wa pili ili kuondoka mkiani mwa msimamo wa ligi kuu ya Uingereza.

Huku wakiwa na alama nne na kushika mkia kwenye msimamo wa ligi kuu ya Uingereza QPR inayofundishwa na kocha Harry Redknapp inahitaji kushinda mechi dhidi ya Liverpool hasa baada ya kuwa na mwanzo mbovu kabisa kwenye ligi, mpaka sasa QPR imeshinda mechi moja , imefungwa mechi 4 na kutoka sare mchezo mmoja .

QPR wamekuwa na rekodi nzuri nyumbani kuliko ugenini kwani katika mechi 7 za mwanzo wa ligi mpaka sasa kati ya mechi tatu walizocheza nyumbani wameshinda mchezo mmoja, wamefungwa mchezo mmoja na kutoka sare mchezo mmoja huku wakipoteza michezo yote minne ya ugenini waliyocheza.

Kocha Redknapp anaweza kuwakosa Joey Barton na Jordon Mutch katika eneo la kiungo huku Niko Kranjcar aliyevunjika kidole cha mguu akitarajiwa kucheza. Wachezaji wa QPR ambao wako tayari kwa mchezo wa leo ni: Green, McCarthy, Hill, Dunne, Ferdinand, Onuoha, Caulker, Yun, Traore, Isla, Henry, Sandro, Fer, Hoilett, Phillips, Kranjcar, Wright-Phillips, Austin, Zamora, Vargas.

Kwa upande wa Liverpool kocha Brendan Rodgers anatarajia kupigana kufa na kupona kupata ushindi wa pili ugenini ili kujiweka kwenye mazingira mazuri ya kupanda na kuwa kati ya timu nne za juu kwenye msimamo wa ligi lakini pia kupunguza tofauti ya alama 12 kati yake na vinara Chelsea.

Habari njema kwa Liverpool inayoshika nafasi ya 10 ikiwa na alama 10 ni kurejea kwa Emre Can na Joe Allen ambao walikuwa wanasumbuliwa na majeruhi hivyo kuongeza makali kwenye kikosi cha “majogoo wa jiji” huku kocha Brendan akisubiria mpaka dakika za mwisho kuamua kama Daniel Sturridge ataweza kuwepo kwenye kikosi kitakachoanza dhidi ya QPR, hii ni baada ya kuwa nje kwa muda na kukosa mechi saba za Liverpool kwenye mashindano mbalimbali.

Hawa ni wachezaji wa Liverpool ambao kocha atachagua wa kuanza kikosi cha leo: Mignolet, Johnson, Skrtel, Lovren, Moreno, Gerrard, Henderson, Lallana, Sterling, Sturridge, Balotelli, Jones, Toure, Manquillo, Enrique, Sakho, Lucas, Allen, Can, Coutinho, Markovic, Lambert, Borini.

Takwimu zinaonyesha Liverpool amecheza na QPR michezo 46 huku Liverpool akishinda michezo 32 na QPR akishinda michezo saba na kwa pamoja wametoka sare mara saba, lakini pia kati ya michezo 13 iliyopita ya ligi ni mchezo mmoja tu wavu wa Liverpool haukutikiswa (clean sheet).

0 comments:

Post a Comment

 
Back to top!