Searching...
Image and video hosting by TinyPic
14 April 2014
Monday, April 14, 2014

WENGER:TUNAHITAJI KUMALIZA NDANI YA NNE BORA


 Na Oscar Oscar Jr
+255789784858

Arsenal wana mechi moja pekee ili kukomesha ukame wa miaka tisa wa kikombe lakini lazima waweke kando mambo ya Kombe la FA watakaporejea uwanjani kupigania nafasi ya kushiriki Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya msimu ujao watakapokuwa wenyeji wa West Ham United Jumanne. 

Ushindi wa Jumamosi wa 4-2 kupitia mikwaju ya penalti dhidi ya mabingwa watetezi Wigan Athletic baada ya sare ya 1-1 hata baada ya muda wa ziada iliwaweka Gunners kwenye fainali ambapo watakutana na Hull City ambayo pia inacheza Ligi ya Premia Mei 17.
Hii ni fursa murua kwao kushinda kombe lao la kwanza tangu ushindi wao wa Kombe la FA 2005.
Ingawa kuchukua kombe hilo katika uwanja wa Wembley bila shaka kutawatia motisha klabu hii ambayo ukakamavu wake mambo yakiwa magumu umetiliwa shaka, kumaliza katika nne bora na kushiriki kwa mara ya 17 mfululizo katika dimba hilo kuu la klabu Ulaya bila shaka kuna umuhimu mkubwa kutokana pia na fedha zinazopatikana huko. 

Kufuatia kichapo cha aibu cha 3-0 mikononi mwa Everton siku nane zilizopita, Arsenal walipoteza nafasi ya nne baada ya klabu hiyo ya Merseyside kuwacharaza Sunderland 1-0 Jumamosi. 

Sasa wako na alama 64, mbili nyuma ya Everton waliosalia na mechi tano, na meneja Arsene Wenger alisema ushindi wa Jumamosi kwenye Kombe la FA utawaweka katika hali nzuri ya kiakili ya kukabiliana na changamoto iliyoko mbele. 

“Ilikuwa nafuu, kila mmoja alikuwa na furaha jana, kwa kufika tu fainali,” Mfaransa huyo aliwaambia wanahabari Jumatatu.
"Jambo lolote tofauti lingeathiri sana hali yetu ya kifikra na sasa kwa sababu tumeweka hilo kando basi tunaweza kuangazia Ligi ya Premia. 

“Ninahisi kwamba tumecheza mechi nyingi sana msimu huu katika dimba tofauti na ngumu pia, lakini tumetia bidii sana katika Ligi ya Premia, na sasa tunataka kumaliza vyema.
"Wana fursa ya kuanza kesho kwa sababu ni mechi kubwa, debi, West Ham wamo kwenye nafasi nzuri kwa maana watacheza bila uoga, kwa hivyo tunajua katika mechi ya aina hii kwamba ni muhimu kubaki na mtazamo mzuri na kazi nzuri kwenye mechi yetu.” 

Arsenal wamekosa kushida katika mechi nne za ligi, huku kichapo cha Everton kikiwa kilitangulizwa na sare dhidi ya Manchester City na Swansea City na kichapo cha 6-0 mikononi mwa Chelsea. 

Huku muda ukiyoyoma, Wenger anakiri kwamba wanahitaji kurejea kwenye kiwango chao cha ufanisi kama wanalenga kuwabandua Everton na kufika Ligi ya Klabu Bingwa, baada ya kushuhudia ndoto ya kushinda ligi ikiyeyuka. 

“Yote yanategemea uendelevu na lazima tuangazie kupata matokeo mazuri na baadaye tuone tutamalizia wapi,” akasema.
“Kiwango cha uchezaji wetu, moyo na pia msimamo wetu (vinanifanya niamini tunaweza kumaliza katika nne bora). 

"Uzoefu unasaidia pia. Lakini tofauti itakuwa ni ubora wa yale unayofanya uwanjani na hilo hutegemea hamu, kuwa mwaminifu kwa uchezaji wetu ambao huwa tunapenda kucheza na pia kuwa na kila mtu tena kwenye kikosi. 

"Ninaamini wana mechi ngumu pia, na tuna mechi ngumu. Tunataka kuangazia sasa yale ambayo tunayojua tunaweza kuyafanya. Tuna kikosi kamili kiasi kwa sasa na tunataka kushinda mechi zetu, bila kujali Everton watafanya nini. Tunataka kumaliza vyema.” 

Kiungo wa kati Tomas Rosicky na beki wa kati Laurent Koscielny huenda wakarudi dhidi ya West Ham walio nambari 11 baada ya kukosa nufusainali hiyo ya Kombe la FA wakiwa na jeraha la paja na misuli ya sehemu ya chini ya mguu mtawalia, lakini Alex Oxlade-Chamberlain (mtoki), beki wa pembeni Nacho Monreal (kufa ganzi mguu) na Aaron Ramsey (kushikana kwa misuli) wanatiliwa shaka, sawa pia na fowadi Lukas Podolski kutocheza mchezo huo.

0 comments:

Post a Comment

 
Back to top!