Searching...
Image and video hosting by TinyPic
30 March 2014
Sunday, March 30, 2014

LIVERPOOL SASA HAWAKAMATIKI



Liverpool walirejea kileleni mwa Ligi ya Premia kwa mara ya kwanza tangu Krismasi kwa ushindi mkubwa wa 4-0 nyumbani dhidi ya Tottenham Hotspur Jumapili. 

Baada ya wapinzani wao Chelsea, Manchester City na Arsenal wote kupoteza alama Jumamosi, Liverpool walitumia vyema fursa hiyo kuimarisha matumaini yao ya kujishindia ligi kwa mara ya kwanza tangu 1990. 

Bao la kujifunga la nahodha wa Tottenham Younes Kaboul liliwafungulia njia Liverpool dakika mbili za kwanza na timu hiyo ya Brendan Rodgers haikurudi nyuma na ilijiwekea hatima ya taji mikononi huku City na Chelsea wakiwa bado watatembea Anfield. 

Mfungaji bora wa mabao msimu huu Luis Suarez aliongeza la pili kwa bao lake la 29 msimu huu baada ya dakika 25, kabla ya Philippe Coutinho kuongeza la tatu dakika 10 baada ya kipindi cha pili kuanza. 

Jordan Henderson alikamilisha kichapo hicho dakika 15 kabla ya mechi kuisha, na kuwakabidhi ushindi wao wa nane mfululizo kwenye ligi. 

Hakuna timu ambayo imezidi rekodi ya Tottenham ya ushindi mara tisa ugenini msimu huu, lakini vijana hao wa Tim Sherwood sasa wamepoteza mechi tatu zilizopita wakiwa nje ya White Hart Lane, huku mambo yao msimu huu yakitishia kuwaendea kombo. 

Lakini huku Spurs wakionekana kuishiwa, Liverpool wanaendelea kuimarika kila uchao wakikaribia kufikia mbio zao za kushinda mechi tisa mfululizo kama walivyofanya msimu wa 2005-06, walipomaliza wa tatu. 

Meneja wa Liverpool Rodgers alifanya badiliko moja tu kwenye timu ambayo ililaza kwenye mechi ya Sunderland 2-1 katikati ya wiki, huku Raheem Sterling akichukua nafasi ya Joe Allen. 

Na Sterling alifanya mambo mara moja kwa kushirikiana na mwenzake wa Uingereza Glen Johnson, ambaye kukimbia kwake kulimpeleka ndani ya eneo la hatari na akatuma krosi ya chini iliyopitia mdomo wa lango. 

Suarez na Daniel Sturridge wote wawili walikuwa wakiusubiri mpira huo kwa hamu, lakini wakapunguziwa kazi baada ya mpira kugonga difenda Jan Vertonghen, na kisha Kaboul alipougusa ukaingia langoni. 

Kuingia kwa Michael Dawson kuchukua nafasi ya Vertonghen aliyekuwa amejeruhiwa hakukufaa kusababisha tatizo kubwa, huku difenda huyo wa muda mrefu akirejesha mpira safu ya ulinzi ya Tottenham akiwa pamoja na Kaboul. 

Lakini kushika kutu kwake kufuatia jeraha kulionekana kwani pasi yake aliyoitoa vibaya iliwezesha Suarez kuufikia na kukimbilia goli. Baada ya kumponyoka Kaboul, straika huyo alimbwaga Hugo Lloris kwa kombora la chini la guu la kushoto ambalo liliingilia kona ya mbali ya goli. 

Hilo lilikuwa bao lake la sita katika mechi nne.
Sterling aliwahangaisha vijana hao wa London sana na dakika nane baada ya kipindi cha pili kuanza, alifaa kuua mechi, lakini badala ya kutoa kombora, akamsambazia mpira Henderson, ambaye kombora lake lilipaa juu ya goli. 

Mwisho hata hivyo haukuwa mbali, kwani dakika chache baadaye Jon Flanagan aliponyoka na mpira eneo la hatari na kumpa Coutinho, ambaye kombora lake la chini kutoka hatua 22 liliingia wavuni kupitia sehemu ya chini kona ya kushoto. 

Henderson baadaye alitoa frikiki kali ya kujipinda kupitia ukuta wa watu lakini ikaenda mikononi mwa Lloris, na kuepusha marudio ya ushindi wa awali wa Liverpool wa 5-0 wakiwa Tottenham mapema msimu huu.

0 comments:

Post a Comment

 
Back to top!